Na. Aron Msigwa –MAELEZO.
Serikali imepiga marufuku matumizi ya Barua pepe za kawaida kwa
watumishi wa umma wanaotuma au kupokea taarifa za Serikali na kuwataka
watumishi hao kuhakikisha kuwa wanatumia mfumo rasmi wa Mawasiliano ya
Barua Pepe Serikalini (GMS) ulioanzishwa na Serikali kwa lengo la
kuimarisha mawasiliano kwa njia ya Mtandao.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es salaam na Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe.Angella Kairuki
alipokuwa akizungumza na Watendaji na Watumishi wa Wakala ya Serikali
Mtandao ( e Government Agency) wakati wa ziara yake ya kukagua utendaji
na ufanisi wa matumizi ya TEHAMA Serikalini.
“Sasa kuna watumishi 7000 wanaotumia anwani za Barua pepe za
Serikali ,idadi hii ni ndogo lazima iongezeke, hatuwezi kuendelea
kuruhusu utumaji wa taarifa za Serikali kwa kutumia Barua Pepe nje ya
mfumo huu” Amesisitiza na kuongeza kuwa Serikali haijakataza matumizi
ya barua pepe za kawaida kwenye mawasiliano binafsi.
Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella
Kairuki (katikati) akiwasili Ofisi za Wakala ya Serikali Mtandao kwa
ziara ya kikazi leo jijini Dar es salaam.
Amesema kwa kutambua umuhimu wa uimarishaji wa mawasiliano ya
TEHAMA Serikalini na kuongezeka kwa matumizi ya TEHAMA katika utumaji wa
taarifa kupitia mitandao mbalimbali ipo haja ya kuweka msisitizo kwa
watumishi wa umma kutumia Barua Pepe za Serikali.
Waziri Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella
Kairuki (kulia) akitembelea maeneo mbalimbali ya Ofisi za Wakala ya
Serikali Mtandao leo. Kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali
Mtandao Dkt. Bakari Jabiri leo alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi
za Wakala hiyo jijini Dar es salaam.
Waziri
Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angella Kairuki
akizungumza na Watendaji na baadhi ya Wafanyakazi wa Wakala ya Serikali
Mtandao leo alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Wakala hiyo
jijini Dar es salaam.
Mhe. Kairuki amewataka watendaji wa Wakala hiyo kuhakikisha kuwa
wanasimamia uratibu wa zoezi hilo ili kuhakikisha kuwa Wizara, Idara na
Taasisi zote za umma zinaunganishwa na mfumo rasmi wa Serikali ili kuwa
na mfumo mmoja wa Mawasiliano.
“Katika hili ninatoa siku 60 muhakikishe kuwa mnakamilisha kwa
Taasisi zilizobaki ili kwa wale watakaopuuzia hatua zianze kuchukuliwa”
Ameeleza Mhe. Angella.
Aidha, ametoa wito kwa watendaji wa Wakala hiyo kuweka mpango wa
kuwawezesha na kuwajengea uwezo wa kitaaluma watumishi waliopo kazini
kwa kujenga utaratibu wa kuwarithisha uzoefu watumishi ili kuendelea
kuimarisha ufanisi na utendaji wa Wakala hiyo.
Mhe. Kairuki amewataka kuwa wabunifu katika kuanzisha mifumo mipya
ya TEHAMA ili kuimarisha dhana ya Serikali mtandao ili kupunguza
gharama hadi kufikia asilimia 5% ya fedha zinazotumika kuendeshea masuala
mbalimbali ambayo yangefanywa kupitia matumizi ya TEHAMA.
Akizungumzia kuhusu ununuzi wa vifaa vya TEHAMA serikalini
ameitaka Wakala hiyo kutoa ushauri ili kudhibiti mianya ya ubadhirifu na
matumizi mabaya ya fedha katika kununulia vifaa hivyo kwa gharama
kubwa wakati vinaweza kupatikana kwa bei ya kawaida.
“katika hili Serikali itachukua hatua kwa yeyote atakayebainika
katika upotevu wa mapato muhakikise mnazisaidia Wizara na Taasisi
mbalimbali za Serikali katika masuala ya ununuzi wa mifumo na vifaa vya
TEHAMA ili mifumo inayonunuliwa iwe na manufaa kwa wananchi na thamani
halisi ya fedha”
Amesema Serikali itaendelea kuboresha utoaji wa huduma kupitia
mtandao ili wananchi waweze kupata huduma hizo mahali walipo kwa
gharama nafuu na kutoa wito kwa watumishi wa Wakala ya Serikali mtandao
(e-Gov) kuwa wabunifu katika kutengeneza programu mbalimbali na mifumo
salama itakayowasaidia wananchi kupata huduma.
Aidha, katika hatua nyingine ameitaka e-Gov kuendelelea kujenga
uwezo katika kudhibiti dharura na majanga mbalimbali yanayoweza
kujitokeza katika matumizi ya TEHAMA na kuitaka Wakala hiyo iendelee
kulifanyia kazi suala la kuwezesha mifumo ya Serikali kuzungumza kati ya
taasisi moja hadi nyingine ili huduma zote ziweze kupatikana katika
eneo moja na kuondoa urudufu wa mifumo iliyopo.
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali Mtandao
(e-Gov) Dkt. Jabiri Bakari akitoa taarifa ya utendaji wa Wakala hiyo
amesema kuwa licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali toka
kuanzishwa kwake Julai 11, 2012 imeendelea kupata ufanisi katika
uimarishaji wa Serikali Mtandao.
Amesema kuwa Wakala hiyo inaendelea kuhakikisha kuwa huduma za
Serikali zinawafikia wananchi kupitia mtandao mahali walipo na
kuhakikisha kuwa inafanikisha lengo la huduma zote za Serikali
kupatikana chini ya dirisha moja.
Aidha amesema kuwa Wakala ya Serikali Mtandao itaendelea
kuhakikisha kuwa usimamizi wa viwango vya matumizi ya TEHAMA katika
Idara na Taasisi mbalimbali za Serikali vinazingatiwa.
@RINYO'S







